Thursday, August 21, 2008

Wabunge wataka muungano ufutwe

MJADALA wa Muungano umeingia katika sura mpya baada ya wabunge kuibua madai ya kutaka iundwe serikali moja ya Muungano badala ya mfumo wa sasa wa serikali mbili.
Kauli hiyo ya wabunge imetolewa wakati tayari Muungano umekuwa ukitikiswa kwa nguvu kutokana na hoja ya Zanzibar si nchi au la.

Wakichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), kwa nyakati tofauti wabunge hao, wengi wao wakiwa wanatoka Bara walisema, dawa pekee ya Muungano huo ni kuundwa kwa serikali moja ya Jamhuri ya Muungano, ingawa dawa hiyo ni chungu.

“Dawa pekee ya Muungano ni kuelekea katika serikali moja ya Jamhuri ya Muungano, ingawa dawa hiyo ni chungu lakini hii ndio italeta Utanzania wa kweli, badala ya kuwa na serikali mbili au tatu,” alisema Mbunge wa Mchinga (CCM), Mudhihir Mudhihir.

Mudhihir alisema, mtafaruku unaoendelea sasa kutokea bungeni, ni mazoea na tamaa za utawala kwa baadhi ya viongozi na kulazimisha kulumbana kwa kugombea majina au serikali kila upande, jambo ambalo halina mantiki kwa sababu majina hayo (Tanganyika na Zanzibar) hakuna anayejua maana yake.

No comments: