Wednesday, October 29, 2008

Jaji Lubuva Astaafu, Aipongeza Serikali

Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Damian Lubuva ameipongeza serikali kwa kudumisha utawala wa sheria na kuipa nafasi Idara ya Mahakama kufanya shughuli zake kwa uhuru bila kuingiliwa na chombo kingine katika mihimili mitatu ya dola. 

Hayo aliyasema jana katika kikao maalumu cha kumuaga katika Ukumbi Namba Moja wa Mahakama Kuu, Dar es Salaam na kuongozwa na Jaji Mkuu Augustino Ramadhani pamoja na majaji wa Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu, mahakimu, mawakili na wanasheria. 

Jaji Lubuva alisema katika Katiba ya nchi, suala la mgawanyo wa madaraka limefafanuliwa vizuri ikiwa ni pamoja na mamlaka na nguvu ya kila mhimili ambayo ni Serikali, Bunge na Mahakama yenyewe. “Ni matumaini yangu kwamba kama mihimili hii mitatu ikiwajibika kwa nafasi yake kwa kuzingatia mipaka ya kazi kwa mujibu wa katiba ni dhahiri Mahakama na Mahakama ya Rufaa zitasimamia vizuri utekelezaji wa sheria katika kutoa haki,” alisema Jaji Lubuva. 

Pia Jaji Lubuva aliwataka mawakili kufanya kazi kwa kuzingatia mipaka ya maadili ya taaluma yao. Naye Jaji Mkuu Ramadhani alimsifu Jaji Lubuva ikiwa ni pamoja na kuelezea historia yake kuanzia enzi za chuoni mpaka hapo alipo sasa. “Niliwahi kukutana na Lubuva supermarket na akaniuliza vipi masomo yako, nilishangaa sana kwa sababu sikujua amejua kuwa nasoma, ila alinijibu tu nimeona paper yako, kwa kweli alikuwa ni mtu mzuri na mwenye kusaidia,” alisema Jaji Mkuu. 

Kwa upande wake, Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika, Dk. Fauz Twaib, mbali na kutaja baadhi ya kesi ambazo zimeshawahi kusimamiwa na Jaji Lubuva, pia alisema ametoa mchango mkubwa katika kusimamia sheria. Dk. Twaib alimkaribisha Jaji Lubuva kujiunga katika chama chao ili kufanya kazi kwa kujitegemea. “Maarifa na hekima zake bado zinahitajika sana katika taaluma yetu, tumependekeza amalize kazi kama jaji kwa kujiunga na chama cha mawakili,” alisema Dk. Twaib. Jaji Lubuva alizaliwa Kondoa mwaka 1940 na kufanya kazi kama mtumishi wa mahakama kwa miaka 15.

Kp Leo

Wahariri Waandamana Dar

WAHARIRI na wadau wengine wa habari nchini, jana waliandamana kutoka mtaa wa Lugoda mpaka Ofisi ya Waziri wa Habari, Michezo na Utamaduni, huku wakiwa wameziba midomo yao kwa plasta. 

Wadau hao walikuwa wakipinga hatua ya Serikali kufungia gazeti la MwanaHALISI huku wakisema bila uhuru wa vyombo vya habari nchini, kashfa za ufisadi kama za Richmond na EPA zingeendelea kulitafuna Taifa. 

Gazeti la MwanaHALISI lilifungiwa na Serikali kwa miezi mitatu, kutokana na kile kilichoelezwa kuandika habari za uchochezi kuhusu njama za baadhi ya viongozi wa CCM kujipanga kumng'oa Rais Jakaya Kikwete madarakani mwaka 2010. 

Wakiwa wamebeba mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali kupinga hatua hizo, wadau hao waliweka historia nchini kwa wanahabari kuandamana kupinga hatua za kuingiliwa uhuru wa vyombo vya habari. 

Baada ya kufika kwenye ofisi za Wizara hiyo, waraka maalumu uliokuwa na ujumbe wa maandamano hayo, ulipokewa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Bw. Habibu Nyundo na kuahidi kuufikisha kwa Waziri husika ambaye kwa sasa yuko bungeni Dodoma. 

Hata hivyo, katika hotuba yake, Bw. Nyundo alidai kuwa Jukwaa la Wahariri halitambuliki kisheria, kwani tayari jina hilo lilishawahi kusajiliwa awali na wahariri wa zamani na aliwataka kubadilisha na kujisajili upya ili watambulike. 

Naye Kaimu Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania Bw. Absalom Kibanda, alisema kitendo cha Serikali kuchukua hatua ya kufungia magazeti ni dalili za wazi za kuishiwa uvumilivu na pengine kuwa mwanzo wa dhamira inayolenga kuendelea kuvibana vyombo huru vya habari, kwa kutumia sheria za zamani kuvikandamiza. 

Naye Mwenyekiti wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika tawi la Tanzania (MISA-Tan), Bw. Ayoub Rioba, alisema hii ni nchi yenye mfumo wa kidemokrasia na inayofuata mfumo wa soko huria, hivyo Serikali haina budi kulinda na kusimamia vyema vyombo vya habari na si kuvikandamiza kwa maslahi ya watu wachache. 

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA), Bibi Ananilea Nkya, alieleza kukerwa na hatua za kufungiwa MwanaHALISI. 

"Ni jambo la hatari kufungia vyombo vya habari kwani kufanya hivyo ni sawa na kuwaziba midomo wananchi ili wasitoe hisia zao kwa manufaa ya Taifa zima," alisema. 

Nacho Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kiliunga mkono maandamano hayo katika ilichokiita salamu zake za mshikamano kwa wanahabari nchini zilizotolewa jana na Mkurugenzi wa Vijana wa Chama hicho, Bw. John Mnyika. 

"Tunawapongeza wahariri kwa mshikamano wenu katika kipindi hiki cha majaribu; endeleeni kusimama pamoja, ni umoja wenu ndio utakaokuwa kinga ya pamoja dhidi ya mtu au chombo chochote kinachoingilia uhuru wenu. 

"Mshikamano wenu ni ishara ya kushindwa kwa mkakati wa ‘wagawe uwatawale’ na imani kwamba umoja ni nguvu. Wahariri wote hawapaswi kukaa kimya kuhusu kufungiwa kwa MwanaHALISI, kwa kuwa leo ni kwa gazeti hilo, kesho itakuwa kwa gazeti lingine; hivyo ni vyema kuungana kulinda uhuru, taaluma na sekta ya habari," alisema. 

Chama hicho kililaumu jinsi hatua hizo zilivyochukuliwa kwa kusema ni sawa na Serikali kuamua kesi ambayo yenyewe ndiyo ilikuwa imelalamika. 

"Hatua ya Waziri mwenye dhamana na sekta ya habari kugeuka mlalamikaji, mwendesha mashitaka na mfungaji ni mwelekeo mbovu wa kupuuza taasisi za kusimamia uwajibikaji na haki. 
"Uamuzi uliofanywa na Serikali hauna tofauti na unaofanywa na raia wanaojichukulia sheria mikononi(mob justice). 

"Kwa Serikali inayoheshimu misingi ya asili ya haki, tulitarajia chombo chochote cha habari, kikivunja sheria ama kukiuka maadili dhidi ya serikali, viongozi wake ama watu binafsi mashitaka au malalamiko yangepelekwa kwa taasisi zinazohusika mathalani Baraza la Habari (MCT) au Mahakama," aliongeza. 

Wakati huo huo, mwandishi wetu Hilary Komba, anaripoti kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Oganaizesheni, Kampeni na Uchaguzi ya NCCR-Mageuzi, Bw. Faustin Sungura, alisema wahariri hawakupaswa kuandamana bila kwanza kujiridhisha iwapo habari iliyosababisha gazeti kufungiwa ilifuata maadili ya kitaaluma na kwamba ilikuwa ya kweli. 

"Maandamano ya wahariri hayakutakiwa kufanyika kabla ya kufanyika uchunguzi wa kina, kwa sababu kwa sasa kuna baadhi ya watu wamejitokeza wanataka kulishitaki gazeti hilo sasa kama litaonekana lina hatia mahakamani basi wahariri watajiweka katika nafasi mbaya," alisema Bw Sungura. 

Kwa maoni yake, alisema wahariri wameharakisha kuandamana kabla hata ya kufanya uchunguzi kwani inaweza kuwashushia hadhi yao, ambayo ni muhimu katika Taifa ambalo linawahitaji kwa kazi zao. 

Alisema wahariri wana haki ya kuandamana kama haki zao zikiwa zimekiukwa kama kufungiwa magazeti, lakini wanapaswa kufahamu kuwa jambo wanalodai lazima liwe limefanyiwa kazi kwanza. 

Aliongeza kuwa iwapo ingebainishwa kwanza ukweli wa habari hiyo, hata chama chake kingekuwa tayari kushirikiana kwa karibu zaidi kupinga hatua iliyochukuliwa ya kulifungia gazeti la MwanaHALISI.

Tuesday, October 28, 2008

Zimbabwe Bado Akieleweki


Maofisa wa serikali ya Zimbabwe wamesema viongozi wa Afrika wanaokutana Zimbabwe wameshindwa kuamua lolote la maana kuumaliza mzozo wa kisiasa wa nchi hiyo.

Mazungumzo ya kugawana madaraka kati ya Robert Mugabe na hasimu wake kiongozi wa upinzani, Morgan Tsvangirai, yamekuwa yakifanyika mjini Harare.

Mchakato wa mazungumzo hayo umekwama kutokana na suala la kugawana wizara muhimu.

Jumuia ya maendeleo ya nchi za kusini mwa Afrika imesema mkutano mkubwa zaidi wa eneo hilo ni muhimu kufanyika kujaribu kumaliza kabisa mzozo wa kisiasa wa Zimbabwe.

Wiki sita zimekwishapita tangu Bwana MUgabe na Bwana Tsvangirai waliposhikana mikono mjini Harare na kutiliana saini kilichoonekana kitendo cha kihistoria cha kugawana madaraka.

Mwandishi wa BBC kusini mwa Afrika Peter Biles amesema jaribio la kuunda serikali ya muungano limeitumbukiza nchi hiyo katika matatizo zaidi.

Siku ya Jumatatu Bwana Mugabe na Bwana Tsvangirai walifanya mazungumzo yaliyodumu kwa saa 13 chini ya muendelezo wa mpatanishi wa mazungumzo hayo, aliyekuwa Rais wa Afrika Kusini na pamoja na viongozi wa Afrika Kusini, Angola, Msumbiji na Swaziland.

Monday, October 27, 2008

Kp Leo

Rostam Aburutwa Kortini


MWANASIASA mashuhuri nchini ambaye pia ni Mbunge wa Igunga (CCM), Bw. Rostam Aziz ameburutwa kortini akitakiwa kulipa mamilioni ya fedha na pia kuomba radhi kwa kile kilichoelezwa kuwa wazazi wake kujihusisha na biashara ya utumwa, limebaini gazeti hili. 

Rostam ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Taifa na Halmashauri Kuu ya Taifa za CCM, kwa hatua hizo sasa atalazimika kufika Mahakama Kuu ya Tanzania mbele ya Jaji Kalegeya Novemba 11 mwaka huu kujitetea kutokana na mashitaka hayo. 

Katika kesi ya madai namba 131 ya mwaka huu iliyofuinguliwa na Mwenyekiti wa Chama cha DP, Mchungaji Christopher Mtikila na Majira kupata nakala yake, Rostam pamoja aliyeunganishwa na magazeti kadhaa nchini yaliyiripoti haba ri hiyo, anadaiwa kumkashifu kiongozi huyo na kutakiwa kulipa sh. bilioni 3. 

Kwa mujibu wa hati ya mashitaka yenye kurasa 10, vipengele 37 na vielelezo lukuki, Mtikila anadai kuwa Bw. Rostam alimchafulia jina na hadhi yake mbele ya jamii kwa maneno aliyoyasema kwenye mkutano wake na waandishi wa habari wa Julai 13 mwaka huu, ambao pia uliripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari zikiwemo tovuti na kuibua mijadala kwenye intaneti. 

"Julai 13 mwaka huu mdaiwa wa kwanza (Rostam) katika mkutano na vyombo vya habari uliofanyika kwenye hoteli ya Kilimanjaro Kempinski alitoa kauli iliyonidhalilisha," inaeleza sehemu ya hati hiyo. 

Maneno ambayo Mtikila anadai kuwa yalimkashifu, yameanza kubainishwa katika katika kipengele cha 12 cha hati hiyo ya mashitaka ikimkariri Bw. Rostam akisema: 

"Matamshi yaliyotolewa wiki hii na Mtikila ni kinyaa, yananuka harufu ya chuki, wivu,ubaguzi,unafiki na ufisadi." 

Chanzo cha sakata hili hadi kutua mahakamani ni tuhuma mbalimbali za ufisadi zinazomkabili Bw. Rostam ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu nchini ambazo baada ya kimya kirefu, alizizungumzia kwa kwa mara ya kwanza alipoalikwa kwenye uzinduzi wa kwaya ya Kanisa la KKT Kinondoni, ambapo mbali na kutoa msaada wa sh. milioni saba, pia alikanusha kuhusika na tuhuma zote hizo na kusisitiza kuwa yeye ni mtu safi mbele ya jamii. 

Siku kadhaa baada ya Rostam kutoa kauli hiyo,Mtikila aliibuka na kulaani kitendo cha Rostam kutoa mchango kanisani na 'kujisafisha' akisema Kanisa halikustahili kupokea fedha za Mbunge huyo. 

Akionekana kukerwa na kitendo hicho, Rostam ndipo alipoitisha mkutano wa Julai 13 ambapo pamoja na kauli iliyoonekana kumuudhi Mtikila alitoa siri kuwa Mchungaji huyo naye aliwahi kumwomba mchango kwa ajili ya kanisa lake na akampa sh. milioni 3. Mtikila hakukana dai ila alihoji uhalali wa risiti ya mchango huo ambayo Rostam aliitoa kwa wanahabari akisema ilighushiwa. 

Katika kesi hiyo, pamoja na kutaka alipwe mamilioni hayo ya fedha Mtikila amembana zaidi Rostam kwa kuiomba Mahakama imwamuru awaombe radhi Watanzania kwa kile Mchungaji huyo alichokisema kuwa ni wazee wa mbunge huyo kujihusisha na biashara ya utumwa. 

Mtikila ameomba katika hati hiyo: "Zaidi (Mahakama) imuamuru mdaiwa wa kwanza (Rostam) aombe radhi kwa maandishi kwa watanzania kwa niaba ya familia yake au mababu zake, kwa kuwafanyia biashara ya utumwa wazee wetu kwa kuwafanyisha kazi za kubeba dhahabu na pembe za ndovu." 

Uchunguzi wa Majira umebaini kuwa dai hilo la Mtikila limetokana na Bw. Rostam kukiri alipozungumza Julai 13 na waandishi wa habari kuwa biashara zake amerithi kwa wazee wake waliokuwa wakifanyabiashara tangu mwaka 1852 ingawa hakutaja aina ya biashara hizo. 

Rostam alisema:"Fedha zangu ni pato halali linalotokana na jasho langu kupitia biashara ambayo imekuwa ikiendeshwa na familia yangu tokea mwaka 1852." 

Kwa mujibu wa Sheria ya Mwqenendo wa Madai na Kanuni za Mahakama Kuu, Rostam halazimiki kufika mwenyewe mahakamani hapo kujitete, iwapo ataamua kuweka wakili au mtu wa kumwakilisha lakini anaweza kulazimika kufika kortini iwapo kuna ushahidi utakaokuwa muhimu yeye mwenyewe kuutoa.

JK Ataka Walimu Walioghushi Waadhibiwe

Rais Jakaya Kikwete ameagiza hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi ya walimu ambao wameghushi au kudanganya wanaidai Serikali wakati hawaidai. Rais ametoa agizo hilo baada ya kuona kuna ongezeko la madai ya walimu kila siku wakati Serikali ilikwisha walipa walimu hao Machi mwaka huu kiasi cha Sh bilioni 7. 

Hatua hiyo imekuja siku chache tu baada ya Rais Kikwete Alhamisi iliyopita kuagiza kuwa madai yote ya walimu yapitiwe upya na ikibidi viongozi wapite shule hadi shule kubaini nani ana madai halali. 

Akitoa agizo hilo baada ya kupokea taarifa ya maendeleo ya Wilaya ya Tabora, Rais alionekana kukerwa na taarifa ya Mkuu wa Wilaya hiyo Moshi Chang’a ambaye alisema walimu wa wilaya hiyo wanaidai Serikali. 

“Deni gani hilo lisilokwisha, haiwezekani tunalipa madeni; lakini yanazidi kuongezeka ama kuna tatizo la viongozi au kuna walimu hawana madai halali,” alisema Rais na kutaka sheria kali zichukuliwe dhidi ya wale watakaobainika kudanganya. 

Rais alitaka ufafanuzi wa madeni hayo ndipo Mkuu wa Wilaya hiyo, Chang’a alisema Msingi wanadai Sh milioni 92.5 kwa ajili ya likizo, posho na uhamisho wakati wale wa Sekondari wanadai Sh milioni 191.8. za posho, matibabu, uhamisho, likizo na malimbikizo ya mishahara. 

“Mheshimiwa Rais baadhi ya changamoto zinazoikabili sekta ya elimu ni pamoja na madeni ya walimu,” alisema Chang’a. Juzi Rais aliagiza kufanyike uhakiki wa madeni ya walimu kuanzia shuleni ili waweze kulipwa haraka. Hivi karibuni walimu walitishia kugoma, lakini mahakama ilizuia mgomo huo kitendo kilichofanya Chama cha Walimu (CWT) wakate rufaa Mahakama ya Rufani.

CCM Wapanga Kumshughulikia Mwanahalisi

JOPO la wenyeviti nane wa mikoa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wameibuka na kusema kuwa wanaenda mahakamani kumshitaki mhariri mtendaji wa gazeti la MwanaHalisi, Saed Kubenea kwa madai kuwa gazeti lake liliandika habari ya kuchonganisha.

Wenyeviti hao, John Guninita wa Mkoa wa Dar es Salaam, Clement Mabina (Mwanza), Khamis Mgeja (Shinyanga), Deo Sanga (Iringa) , Onesmo Kangole (Arusha), Hypolitus Matete (Rukwa), Nawab Mulla (Mbeya) na William Kusila (Dodoma), wamechukua hatua hiyo siku chache baada ya serikali kulifungia gazeti hilo kwa miezi mitatu.

Serikali iliamua kufungia gazeti la MwanaHalisi baada ya kuandika habari iliyoelezea harakati zinazoandaliwa za kumuondoa Mwenyekiti wa CCM, Rais Kikwete kwenye mchakato wa kuwania urais kupitia chama hicho kwenye uchaguzi wa mwaka 2010, akiitaja mikoa hiyo kuwemo kwenye mipango hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya wenyeviti wenzake katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika kwenye jengo la CCM la mkoa jana, Guninita alisema habari hiyo imewasikitisha sana na wanaenda mahakamani kumfungulia kesi mwandishi na kudai fidia.

“Kwa kuwa Kubenea hakututendea haki kwa kutuingiza katika tuhuma nzito ambazo sio za kweli, sisi viongozi nane kama alivyotutaja kwa majina tumeamua kumfikisha mahakamani,” alisema Guninita.

Alisema tayari wameshazungumza na mawakili wao ambao hakuwataja na kwamba muda wowote kuanzia leo Kubenea ataitwa mahakamani.

Alifafanua kuwa kutokana na tafsiri yao kuhusu habari hiyo, wameona kuwa Kubenea anataka kuwagombanisha na mwenyekiti wao, Rais Jakaya Kikwete kuwa wana mpango wa kumng'oa.

Alisema kwamba Kubenea amewapaka matope na kuwafanya wasiaminike kwa viongozi wenzao pamoja na wanachama wenzao wa CCM.

Guninita alieleza kuwa habari iliyochapishwa katika gazeti la MwanaHalisi toleo namba 118 la Oktoba 14 yenye kichwa cha habari ‘Njama za kumng’oa Kikwete zafichuka’ iliyoandikwa na Kubenea ilikiuka maadili ya uandishi.

Alisema lengo la kwenda mahakamani ni kumtaka Kubenea athibitishe ukweli mbele ya sheria juu ya uzushi, uchochezi, na uongo wake mbele ya wananchi ili waweze kuona dhahiri uongo wa madai yake.

“Pia tutadai fidia, kuhusu kiwango... hilo ni suala la kisheria na baada ya kushauriana na mawakili wetu tutajua ni kiasi gani tutadai,” alisema Guninita.

Guninita alikanusha vikali kwa niaba ya viongozi wenzake, kuhusika na taarifa hiyo na kuiita kuwa ni ya kizushi, uchochezi na uongo mtupu.

“Kubenea ameandika habari hizo kwa maslahi yake binafsi na sisi hatuhusiki na taarifa hizo za uongo. Bado ni viongozi watiifu kwa mwenyekiti wetu pamoja na chama chetu kwa ujumla,” alilalamika Guninita.

Akiongea na Mwananchi, Kubenea alisema njia iko wazi kwa wenyeviti hao kama wanataka kwenda mahakamani na kuongeza kuwa hawatapata kitu.

Alisema hizo ni katika harakati za kujikosha kwa mwenyekiti wa taifa wa CCM na kwamba yeye hana wasiwasi wowote juu ya vitisho vyao.

“Kama wanaenda na waende, lakini watashindwa tu, huko ni katika kujikosha na mimi sina wasiwasi,” alisema Kubenea.

Bunge Kenya lataka tume ya maridhiano

Bunge la Kenya limepitisha muswada wa kuanzishwa tume ya ukweli, haki na maridhiano (TJRC), kuchunguza visa vya kukiukwa kwa haki za binadamu tangu nchi hiyo ilipojinyakulia uhuru, mwaka 1963.

Wale ambao itathibitishwa walihusika katika visa vya mauaji ya watu wengi na kukiuka haki nyinginezo za kibinadamu kamwe hawatapata fursa ya msamaha.

Hatua hiyo imeafikiwa huku kukiwa na mjadala ni vipi nchi hiyo itakabiliana na wale ambao walihusishwa na ghasia zilizozuka mara tu baada ya uchaguzi uliozusha utata mwezi Desemba mwaka 2007.

Tume ya kimataifa imehimizwa kuwafungulia mashtaka waliohusika katika kupanga ghasia hizo.

Zaidi ya watu 1,500 waliuawa, na wengine zaidi ya 300,000 kuyakimbia makao yao kutokana na mapigano yaliyozuka.

Rais Mwai Kibaki, na kiongozi wa upinzani wa Orange Democratic Movement, Raila Odinga, ambaye sasa ni waziri mkuu, walitia saini makubaliano ya serikali ya uongozi wa pamoja mwezi Februari, katika juhudi za kukomesha ghasia hizo.

Kuanzishwa kwa tume ya maridhiano (TJRC) ni kufuatia mapendekezo ya tume nyengine iliyoanzishwa kuchunguza kiini hasa cha kuzuka kwa ghasia na machafuko hayo ya kisiasa.

Friday, October 24, 2008

Wednesday, October 22, 2008

Tanzania's First


Dar es Salaam, Tanzania: October 20, 2008: Vodacom Tanzania has officially launched BlackBerry smartphones Curv 8310 and Pearl 8110 exclusively to prepaid and postpaid customers, making the first mobile network in Tanzania to introduce BlackBerry smartphones to prepaid customers.

BlackBerry on Postpaid
  • Get a BlackBerry smartphone! 
  • Add BlackBerry Internet Service (BIS) or BlackBerry Enterprise Solution (BES) to an existing or new Vodacom Postpaid account. 
  • Enjoy UNLIMITED monthly access to email and Internet browsing on your smartphone!

*Available on Vodachoice, Talk 200, Talk 500 and Talk 1,000 packages.

BlackBerry on Prepaid
  • Get a BlackBerry smartphone! 
  • Purchase a Prepaid BlacBerry Internet susbcription via SMS, vouchers or VodaFasta for 30, 90 or 180 days. 
  • Enjoy UNLIMITED access to email and Internet browsing on your smartphone! 

**Available on Prepaid and VodaJaza, for company accounts, contacts:
corporatesolutions@vodacom.co.tz

Prepaid & VodaJaza susbcriptions from Vodacom

To subscribe, SMS the below keyword to 123

  • BLACKBERRY1 for Tsh 36,000 to be used within 30 days 
  • BLACKBERRY3 for Tsh 99,000 to be used within 90 days 
  • BLACKBERRY6 for Tsh 180,000 to be used within 180 days 
*Download mpaka uchoke kwa mwezi au miezi kwa kiwango kimoja.

Kp Leo

Dk. Shein aonya matumizi mabaya ya madaraka


Makamu wa Rais, Dk. Ali Mohammed Shein ametahadharisha juu ya matumizi mabaya ya madaraka katika halmashauri na kuwataka viongozi na watendaji kuziendesha kwa kuzingatia misingi ya utawala bora. 

“Sheria na kanuni zifuatwe pasiwe na ubabe katika halmashauri na taasisi za serikali, tukifanya hivyo tutakuwa tumezingatia utawala bora,” alisema na kusisitiza kuwa kwa wale ambao wawejisahau hapana budi wakakumbushwa, lakini alionya kuwa pindi wasiposikia wasisite kuchukuliwa hatua zifaazo. 

Dk. Shein alitoa tahadhari hiyo juzi wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa Mkoa wa Arusha kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), akihitimisha ziara yake ya siku saba. 

“Hakuna aliye juu ya sheria, si Mwenyekiti, Mkurugenzi wala diwani wote tunapaswa kufuata sheria na taratibu zinazoendana na madaraka tuliyopewa. Tutekeleze mipango tuliyoipanga katika vikao vyetu kutekeleza wajibu wa kuwatumikia wananchi,” alisema Dk. Shein. 

Alisema halmashauri si mahali ambako kila kiongozi anaweza kuleta ajenda au mipango yake kutekelezwa na kuzitaka kutenda haki katika kuwahudumia wananchi kwa kutoruhusu upendeleo. Katika mkutano huo, Makamu wa Rais aliwakumbusha viongozi wa mkoa huo kutekeleza wajibu wao kwa ushirikiano na kujenga mshikamano na upendo miongoni mwao na kuongeza kuwa uongozi wa pamoja unaepusha kulaumiana miongoni mwa viongozi. 

“Ni muhimu kuimarisha uongozi wa pamoja kwa kushauriana na kuonyesha mshikamano miongoni mwenu na katika mazingira kama hayo hata pale mambo yanapokwenda kombo kila mmoja atasita kumlaumu mwenzake,” alisema na kueleza kuridhishwa na jitihada za viongozi na watendaji katika utekelezaji wa majukumu yao pamoja na juhudi za wananchi wa Arusha katika kujiletea maendeleo. 

Dk. Shein ambaye alitembelea wilaya zote isipokuwa Ngorongoro, hata hivyo, aliutaka uongozi wa mkoa na wilaya kupanga mikakati bora zaidi ya kuimarisha kilimo cha kisasa na ufugaji bora ambao tayari umeonyesha mafanikio katika baadhi ya sehemu mkoani humo. 

Aliwataka viongozi na watendaji wa Mkoa wa Arusha kutekeleza mpango wa uimarishaji wa sekta ya kilimo mkoani humo kwa kuzingatia uongezaji tija kwa kutumia njia bora za kilimo pamoja na matumizi ya mbegu bora na kuimarisha kilimo cha umwagiliaji

Vyama vya siasa vyadai mwafaka ni mradi wa CCM na CUF

VIONGOZI wa vyama vya siasa nchini wamevishutumu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Wananchi (CUF) kuwa wanaendekeza ufisadi kwa kisingizio cha mazungumzo ya kutafuta mwafaka wa kisiasa visiwani Zanzibar kila unapomaliza uchaguzi mkuu.

Mwenyekiti wa National League for Democracy (NLD) Dk Emmanuel Makaidi alidai kusa CCM na CUF hawana ugomvi wowote isipokuwa wana mradi wao wa kifisadi wa

kutafuta fedha kwa kupitia mwafaka.

Mwenyekiti huyo aliyasema hayo katika warsha ya siku mbili ya viongozi wa kitaifa wa

vyama vya kisiasa nchini inayofanyika katika hoteli ya Bwawani iliyoandaliwa na Mpango wa Utafiti na Elimu ya Demokrasia Tanzania (REDET).

Dk Makaida alisema anashangazwa vyama hivyo kung’ang’ania kutatua wanchodai kuwa ni mgogoro wa Zanzibar pasipo kushirikisha vyama vyengine vya siasa vilivyosajiliwa kwa mujibu wa sheria na kusisitzia kuwa visiwani humo hakuna vyama viwili kama ambavyo CCM na CUF wanataka ionekane.

“Kwani nini wanangangania vyama viwili kufanya mazungumzo yasiokwisha na kila baada

ya uchaguzi mkuu wafadhili wanakutana na kutoa fedha kwa ajili ya kazi hiyo. Huu ni ufisadi…samahani kwa kusema hayo,” alisema Makaidi.

Alisema kitu ambacho hakubaliani nacho ni CUF kuandaa maandamano kudai serikali ya mseto huku wakitambua kuwa wao wana nafasi katika bunge, hivyo walipaswa

kwanza kuwafichua mafisadi wanaorejesha nyuma maendeleo ya nchi.

Mwakilishi wa Chama Cha Sauti ya Umma (SAU), Peter Mwagira alisema kwamba hawakubaliani na mgogoro unaozushwa na CCM na CUF visiwani Zanzibar kwani mgogoro huo ni wa kupika kwa lengo la kuwanufaisha vyama hivyo viwili.

Alisema mgogoro uliopo ni baina ya vyama vyengine vya kisiasa dhidi ya CCM na CUF ambao unatakiwa kushughulikiwa haraka iwezekanavyo.

Viongozi wengine waliochangai mada hiyo ni Victor Manyai aliyedai kuwa CUF na CCM vinageuza mazungumzo ya kutafuta mwafaka kuwa ni mgodi wao.

Naye Mwenyekiti wa Chama Cha TADEA, Dustan Lifa Chipaka alidai kuwa CCM na CUF walikula njama katika kuharibu mwafaka wa kisiasa visiwani Zanzibar na kwamba mchakato wa mazungumzo hayo ni kiini macho.

Wakitoa mada katika warsha hiyo juu ya migogoro na utatuzi wake ndani ya vyama na suluhisho la migogoro baina ya vyama Tanzania, wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Professa Mohabe Nyirabu na Bashiru Ally walielezea udhaifu unaosababisha hali hiyo.

Professa Nyirabu alisema kuwa tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 kumekuwa na migogoro mingi na kwamba uhai wa baadhi ya vyama unatatemea nguvu na uwezo wa waanzilishi wake.

Naye Profesa Bashiru alisema kuwa vyama vingi vimeingia katika migogoro baina yao kutokana na kukiuka misingi ya demokrasia na kutoheshimu taratibu walizojiwekea.

Hongera Sana Ndugu


Amiri Jeshi Mkuu Rais Jakaya Kikwete akimpongeza na kumzawadia mwanafunzi bora katika mafunzo ya maofisa wa jeshi, Luteni Usu Israel Mwashala, wakati wa sherehe za kuwatunuku kamisheni maofisa wapya wa jeshi waliohitimu mafunzo ya mwaka mmoja katika Chuo cha Jeshi Monduli mkoani Arusha jana. 

Obama asitisha kampeni kumwuguza bibi


Mgombea kiti cha urais wa Marekani kupitia chama cha Democratic, Seneta Barack Obama, ametangaza kuweka kando shughuli za kampeni kwa muda aweze kwenda Hawaii kumwangalia bibi (nyanya) yake ambaye ni mgonjwa.

Tangazo hilo limetolewa na maafisa wake huku Bw Obama akipiga kampeni katika jimbo la Florida, ikiwa ni pamoja na kufanya mkutano bega kwa bega na Hilary Clinton, aliyekuwa hasimu wake katika kura za maoni ndani ya chama cha Democratic.

Kampeni ya Bw Obama imeeleza kuwa kuanzia siku ya Alhamisi mgombea huyo ataacha kampeni ikiendelea na kwenda kumtembelea bibi (nyanya) yake, Madelyn Dunham, mwenye umri wa miaka 85.

Ugonjwa
Maafisa wake wamebainisha kuwa ingawa Bw Obama mwenyewe hatakuwepo lakini kampeni zitaendelea kama kawaida, atawakilishwa na watu wanaomwunga mkono akiwemo mkewe Michelle Obama.

Bw Obama ataahirisha shughuli alizokuwa afanye katika mji wa Des Moines jimbo la Iowa na Madison, kwenye jimbo la Wisconsin.

Hali ya bibi yake Bi Dunham, aliyesaidia kwa kiasi kikubwa kumkuza na kumlea Barack, haifahamiki bayana, ingawa mpambe mmoja Bw Robert Gibbs amesema afya yake imekuwa ikidhoofika katika majuma ya karibuni.

Vijembe
Katika mojawapo yake ya hotuba zake aliahidi kupinga hatua za kuwaondoa watu majumbani mwao kwa sababu wameshindwa kulipa mikopo ya kununua nyumba.

Kwa upande mwingine, mgombea wa chama cha Republican, John McCain amekosoa sera za uchumi za hasimu wake akiapa kupeleka nchi katika mweleko mpya.

Akipiga kampeni huko Missouri, jimbo jingine linalogombewa na vyama vyote, John McCain alimshutumu mpinzani wake wa Democratic kwa kuwapotosha wananchi kuhusu mipango yake ya kuongeza kodi.

Kampeni ya Barack Obama imepata nguvu kutokana na Collin Powell aliyewahi kuwa waziri wa mambo ya nje katika serikali ya rais Bush kutangaza kumwunga mkono na kumtosa mgombea John McCain wa chama chake cha Republican.

Monday, October 20, 2008

Kp Leo

Maalbino Waandamana Dar

Baadhi ya washiriki wakiandamana kupinga mauaji ya Maalbino nchini, yaliyoanzia jana Shule ya Uhuru Mchanganyiko na kupokelewa na Rais Jakaya Kikwete kwenye viwanja vya Karimjee, Dar es Salaam.

Rais Jakaya Kikwete akiteta na Mwenyekiti wa Chama cha Maalbino, Ernest Kimaya, baada ya kupokea maandamano ya kupinga mauaji yao yaliyofanyika jana Dar es Salaam.

Saturday, October 18, 2008

Annan aipokea ripoti juu ya ghasia Kenya

Katibu mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, na ambaye aliongoza shughuli za upatanishi kufuatia mgogoro wa kisiasa nchini Kenya, ameipokea ripoti ya tume iliyochunguza ghasia nchini humu kufuatia uchaguzi wa rais mwaka jana.

Bw Annan aliipongeza tume hiyo iliyosimamiwa na Jaji Waki, akisema ilitekeleza kazi nzuri.

Alisema ataitisha mkutano kati yake na Rais Mwai Kibaki, na Waziri Mkuu Raila Odinga, ili kushauriana juu ya hatua zitakazofaa.

Uchunguzi wa tume hiyo utaendelewa kuhifadhiwa kwa siri, hadi pale hatua muwafaka zitahitajika kuchukuliwa.

Bw Annan alielezea kwamba anafahamu kuna hisia miongoni mwa wengi kutaka kujua ni nani aliyetajwa, au hakutajwa katika uchunguzi wa tume hiyo, lakini alisema ni vyema kuepuka kuwaza hayo, hadi pale kiongozi wa mashtaka, au jaji atakapofungua kesi na kuanza kazi yake.

Alielezea kwamba ni muhimu kufuatia utaratibu unaofaa, hasa katika kuheshimu haki za mtu binafsi, na hii sio mara ya kwanza kuzingatia utaratibu kama huo.

Alisema anaamini ikiwa wote wataheshimu na kuzingatia utaratibu huo, basi utekelezaji utawezekana.

Friday, October 17, 2008

John Meli Aelezea Yaliyomsibu

UNAPOKUTANA na John Meli (55), mara moja utabaini kuwa ni mtu aliyekata tamaa ya kuishi.

Ni kutokana na maisha yanavyomwendea kombo. Ni mlemavu wa mikono yote miwili, ulemavu alioupata ukubwani kiasi cha kumfanya ashindwe kujitegemea kama alivyozoea alipokuwa mtumishi wa Shirika la Reli Tanzania(TRC).

Meli hawezi kukumbuka vizuri hali ilikuwaje hadi akapata ulemavu huo ingawa anajua kuwa mikono yake miwili ilikatwa na mashine.

“Siwezi kusema kwa hakika ni nini kilitokea zaidi ya kuwa nilipostuka, niliona mkono wangu wa kushoto ukiwa tayari umenaswa na mashine na kuvunjika. Nikiwa nimetaharuki nikajikuta natumia mkono wangu wa kulia kuunasua mkono wangu, kumbe ndio nilikuwa najiongezea matatizo makubwa zaidi; mkono wa kulia nao ulikatwa mara moja," anasem Meli.

Alikuwa mfanyakazi wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) tangu mwaka 1975 akiwa katika idara ya ufundi. Alitumikia shirika hilo kwa miaka mitano kabla ya kukumbwa na ajali hiyo kubwa iliyomvurugia ndoto ya maisha yake.

"Nilikuwa nikifanya kazi katika karakana ya kituo kikuu cha reli mkoani Tabora," anakumbuka.

"Huko nilikuwa nikichonga vipuri vilivyohitaajika kwa ajili ya mashine za kupandishia mizigo melini kule Mwanza.

"Siku hiyo wafanyakazi wenzangu walikuwa wamekwenda kula chakula cha mchana. Mimi nilitaka kukamilisha kazi zangu kwanza ndipo niende kuungana nao katika chakula.

"Siwezi kukumbuka vizuri ilitokeaje lakini katika kujaribu kumaliza kazi zangu mapema, nilistukia nimeingiza mkono kwenye mashine na baadaye nikaingiza mkono wa pili na kuupoteza mkono wa kulia, huku mwingine ukiwa umeumia vibaya.

"Sasa naishi kwa kutegemea huruma za watu."

Tukio hilo lilitokea Januari 18, 1980 na baada ya kukatika mikono yote, alikimbizwa hospitali ya Mkoa ya Kitete kwa ajili ya kupata matibabu, lakini tayari "nilikua nimeshaharibikiwa kimaisha".

“Maumivu yalipokuwa yakipungua, nililazimika kuanza kufanya mazoezi ya kuandika kwa kutumia mkono wa kushoto ambao ulipona baadaye. Nilipopata kasi katika kuandika nilibadilishiwa kazi na kuwa karani, kazi ambayo niliifanya kwa ufanisi mkubwa,” anasema mfanyakazi huyo wa zamani wa TRC.

"Hata hivyo, kuna wakati anapata maumivu makali kutoka katika mikono yote miwili, hasa mkono naoandikia na hivyo kuendelea kupata mateso.

“Nadhani pia suala hilo liliingiliana na ile hali ya Ustawi wa Jamii wizara kutoa ufadhili wa mimi kupata mkono wa bandia, kwani kulijenga chuki kutoka kwa baadhi ya watu pale ofisini, wengine wakitaka niwape kitu kidogo.

"Nitawezaje kuwasomesha hawa, hasa Jennifer ambaye yuko kidato cha pili na Ezekiel ambaye yuko kidato cha kwanza," anasema.

“Mahali pa kulala sina shida, na fedha za kujikimu sina. Hivi sasa sasa walau Manispaa ya Dodoma imenisaidia kulipa karo ya wanangu. Wakitoka shule wakati mwingine kunakuwa hakuna chakula, na ninavyoona ni kuwa wanangu wanateseka sana,” anasema Meli.

"Angalau tunaweza kupata Sh1,000 kwa siku, hata kama haikishi mahitaji, inasaidia kukabiliana na tatizo la wakati huo," anasema.

“Nimekata tamaa sana. Natamani hata kujitupa katika gari nife, lakini najua itawaoongezea ugumu wa maisha wanangu.Kwa hakika naomba nisaidiwe mtaji wa kufanya biashara ndogondogo.

"Suala la msingi niwe na fedha iwapo mmoja wa wana familia wangu anaumwa asikose matibabu.”

Akiangalia hali yake, Meli anaona kuwa mashirika na makampuni yao wajibu wa kutathmini sera zao kuhusu watu wanaokutwa na matatizo kama yake.

"Ni vyema kuwa karibu na mtu wa aina hiyo ili kumudu kumsaidia kuendeleza maisha," anasema. "Si vizuri kuwapunguza kazini kwa sababu inakuwa kama ni kuwakomoa.

"Mashirika makubwa kama TRC, Tanesco na mengineyo ni vyema yaige mfano Amboni ambayo mmoja wa wafanyakazi wake alipopata ajali na kukatika mkono, alipangiwa kazi ya kufungua mlango getini alipoonekana ameshindwa kuendelea na majukumu yake ya zamani.

Meli, hata hivyo, hakuondoka kavukavu TRC. Alipata kiinua mgongo kilichomfanya anunue nyumba anayoishi hivi sasa.

Alilipwa Sh16 milioni, ikiwa ni mafao yake yote, lakini akalipwa kifuta jasho cha Sh30,000 mwaka 2003 baada ya kupunguzwa kazi mwaka 1981.

Mzee huyo anayeishi katika eneo la Nkuhungu anawaomba wasamaria wema kumsaidia kupata mtaji wa biashara ndogondogo zitakazoendana na ulemavu alionao, akiamini biashara ya duka dogo linaweza kumsaidia kuendesha maisha yake.


Muafaka Wakaribia Kufikiwa Zimbabwe

Rais wa Zimbabwe, Robert Mugabe, na afisa mwandamizi mmoja wa upinzani wamesema muafaka wa kugawana madaraka utafikiwa baada ya muda mfupi.

Gazeti linalomilikiwa na serikali ya nchi hiyo, The Herald limeandika kwamba afisa mmoja wa Bw Mugabe alisema nyadhifa zilizopangwa wiki iliyopita huenda zikabadilishwa.

Hata hivyo, kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai hakuwa na matumaini makubwa akisema mazungumzo hayo yamekuwa ya ubabaishaji.

Aliyekuwa rais wa Afrika Kusini Thabo Mbeki amekuwa akisimamia mazungumzo hayo kwa siku ya pili sasa.

Bw Mugabe na Bw Tsvangirai walitia saini ya mpango wa kugawana madaraka mwezi uliopita.

Lakini viongozi hao wameshindwa kufikia makubaliano ya kugawana nyadhifa katika wizara mbalimbali nchini humo hadi sasa.

Chanjo ya Kupooza Yaleta Matumaini

Ugonjwa wa kupooza unaweza ukatoweka kabisa nchini Nigeria, moja ya maeneo ya mwisho hapa duniani yanayoendelea yanayokumbwa na maradhi hayo.

Watafiti wanasema sababu ya kutoweka ugonjwa huo ni chanjo yake kuboreshwa zaidi.

Watafiti wa chuo cha Imperial cha London kimegundua chanjo iliyozinduliwa hivi karibuni ina uwezo wa zaidi ya mara nne kuwalinda watoto kuliko chanjo za awali.

Wataalamu hao walisema chanjo hiyo inaweza ikatokomeza kabisa 'type 1 polio' inayojulikana zaidi nchini humo iwapo itawafikiwa watoto wengi.

Nigeria ni moja ya nchi nne tu duniani ambayo bado ugonjwa huo haujatokomezwa.

Asilimia 82 ya kesi za maradhi hayo imeripotiwa kuwepo nchini Nigeria.

Ugonjwa huo una athari kubwa sana na huwadhuru watoto walio chini ya umri wa miaka mitano.

Thursday, October 16, 2008

Hivi Polisi Wapokugonga Inakuwaje

Gari la polisi wa usalama Barabarani lenye namba za usajili PT 0310 likiwa limeligonga gari lenye namba za usajili T673 AHK juzi kwenye eneo la uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.

Walimu Wagoma Kibaridi


KAMA sheria mpya ya kazi ina mtihani mkubwa wa kwanza tangu ianze kutumika mwaka 2006, basi uamuzi wa jana ndio mtihani mwafaka baada ya walimu katika mikoa mingi nchini, kupuuza amri ya mahakama ya kuzuia mgomo na kutekeleza dhamira yao kwa njia tofauti.

Jumatatu, Jaji William Mandia wa Mahakama ya Kazi alitoa uamuzi wa kuzuia mgomo wa walimu, baada ya kuridhika kuwa mgomo huo ungeathiri sekta nzima ya elimu na hasa wanafunzi ambao wanaendelea na mtihani wa taifa wa kumaliza kidato cha nne. Jaji huyo alitoa amri hiyo baada ya serikali kufungua kesi na kuwasilisha ombi la kuzuia mgomo huo uliopangwa kuanza jana.

"Tumechukizwa sana na kitendo cha serikali kutaka kutuziba midomo kwa kwenda mahakamani. Sasa sisi walimu wa Tarime tunawaomba waje kutufukuza kazi wote," alisema mwenyekiti wa CWT wilayani Tarime, Matinde Magabe.

"Ni aibu kwa serikali kwenda mahakamani eti kuzuia mgomo. Sasa wao waje kufundisha huku vijijini, si wanatudharau sisi."

Naye mwalimu aliyejitambulisha kwa jina la Hassan wa wilayani Tarime alimwambia mwandishi wetu akisema: “Mimi nimekasirika sana kuona serikali inakwenda mahakamani kuweka pingamizi ili tusidai haki yetu. Hivi hawa viongozi kwa kuwa wanaona mambo yao yanawaendea vizuri kutokana na kusomesha watoto wao shule za nje, ndio wanakuwa hawana uchungu na walimu wa Tanzania.”

Walimu hao wanaidai serikali zaidi ya Sh16 bilioni, ikiwa ni sehemu ya Sh23 bilioni ambazo wafanyakazi wanaidai serikali. Limbikizo hilo la fedha za walimu linatokana na fedha za nauli, posho mbalimbali, fedha za uhamisho, huku baadhi ya walimu wakidai kupandishwa madaraja.

Wakati walimu wakianza mgomo huo baridi, chama chao cha taifa jana kilikuwa kikihaha kuwasilisha rufaa yao kwenye Mahakama ya Rufaa kutaka amri hiyo ya Jaji Mandia iondolewe ili waanze mgomo kama ilivyopangwa.

"Tunawasilisha rufaa yetu kesho (leo) na tutasubiri uamuzi iwapo itapita, tutatangaza kuanza mgomo mara moja," alisema mwanasheria wa CWT, Leonard Haule.

"Mgomo wetu ulifuata sheria zote na hivyo ulikuwa halali, lakini mahakama ilizuia kwa muda tu. Walimu lazima waelewe kuwa mgomo haujafutwa, bali umesimamishwa na mahakama. Kwa hiyo rufaa yetu ikishinda, tutaendelea kama ilivyopangwa."

Paulina David kutoka Mwanza anaripoti kuwa, walimu walikuwa wakiimba nyimbo za kutiana nguvu wakati walipokutana kwenye viwanja vya Ghandhi kuanza mgomo.

"Kama sio juhudi zetu walimu... na Kikwete angetoka wapi. Kama siyo juhudi zetu walimu... na majaji wangetoka wapi. Kama siyo juhudi zetu walimu na Maghembe angetoka wapi," ndivyo walivyoimba walimu hao jana.

Walimu hao walikubaliana kuwa wasiende kabisa kazini jana na kwamba leo waende kutia saini tu halafu waondoke bila ya kufanya kazi, lakini Ijumaa wakutane tena kwenye viwanja vya Ghandhi na kujadili mambo yao.

“Tunatoka hapa kwenda nyumbani kulala kesho tunakwenda kusaini kwenye kitabu cha mahudhurio, keshokutwa tunarudi hapa hapa kuendelea na mazungumzo yetu,” alisema mmoja wa walimu

Mwenyekiti wa CWT wa Mwanza, John Kafimbi, alisema kuwa walikataliwa kutumia Ukumbi wa Ghandhi na wamiliki wake waliosema kuwa kutumia ukumbi huo kungemaanisha wamiliki hao kubariki mgomo.

Jijini Dar es salaam, Patricia Kimelemeta anaripoti kuwa walimu walikuwa wakiendesha mgomo baridi baada ya kuripoti kwenye vituo vya vya kazi, lakini wakaamua kutoingia darasani.

Katika baadhi ya shule, walimu hao waliwatangazia wanafunzi wao kuwa hawangeingia madarasani kutokana na sababu zao.

Katika Shule ya Msingi ya Makuburi iliyopo Manispaa ya Kinondoni, walimu hawakuingia madarasani.

“Tumetangaziwa mstarini kuwa walimu hawaingii madarasani kutokana na sababu zao, hivyo basi tumeshindwa kufanya mtihani wa moko na mpaka sasa hatujafundishwa somo lolote na muda wa kuondoka umefika,” alisema mwanafunzi mmoja wa shule hiyo.

Shule nyingine zilizokumbwa na sakata hilo ni Shule ya Msingi Mabibo na Mlimani zilizo Kinondoni wakati kwenye Manispaa ya Ilala ni Shule ya Msingi ya Ulongoni.

Naye Mussa Juma kutoka Tarime anaripoti kuwa zaidi ya walimu 800 walianza mgomo wa kuingia madarasani baada ya uamuzi wa kuridhia mgomo huo kufikiwa jana kwenye Shule ya Msingi ya Turwa.

Walimu hao wanaidai serikali zaidi ya Sh400 milioni.

Akizungumza na Mwananchi baada ya kikao hicho, mwenyekiti wa CWT wilayani Tarime, Matinde Magabe alisema wamekubaliana kuanzia jana kuacha kufundisha.

Mwenyekiti huyo alisema walimu wa wilaya hiyo ya Tarime na wilaya mpya ya Rorya watakuwa wakifika shuleni na kusaini daftari na baadaye kurejea majumbani.

Alisema walimu wa Tarime pekee wanaidai serikali jumla ya Sh236 milioni wakati wa Rorya wakiwa wanadai Sh178 milioni, fedha ambazo ni malimbikizo ya madai mbalimbali.

Mwenyekiti huyo alisema malimbikizo hayo ni pamoja na malipo ya usafiri, likizo, nyongeza za mishahara na malipo mengine ambayo yapo katika mikataba yao ya ajira.

"Pia hapa kuna walimu zaidi ya 500 hawajawahi kupandishwa madaraja hivyo tuna kila sababu ya kuanza mgomo huu," alisema Magabe na kusisitiza kuwa mgomo utaisha pale tu watakapolipwa madai yao yote.

Kutoka Serengeti, Anthony Mayunga anaripoti kuwa walimu katika kata za Issenye, Kisangura, Manchira, Mugumu Mjini, Rung'abure, Machochwe, Ikoma na Kyambahi, waliohojiwa kwa nyakati tofauti, walikiri kuwepo mgomo baridi licha ya serikali kusambaza waraka kuwasihi wasigome.

"Inachofanya serikali ni mchezo wa kuigiza kwa kuwa unaweza kulazimisha punda kwenda mtoni, lakini huwezi kumlazimisha kunywa maji," alisema mwalimu mmoja akimaanisha amri ya Mahakama Kuu kutaka wasigome na uamuzi wao wa kwenda kazini bila ya kufundisha.

Katibu wa CWT wilayani, Wanjala Nyeoja alidai kuwa mgomo baridi unaoendelea ni ishara tosha kuwa walimu wamekata tamaa, wamechoka kuona wanasiasa wananeemeka kwa njia za propogandaa, wakati afisa elimu wilaya, Ishengoma Kyaruzi alidai kuwa alikuwa anafuatilia mashuleni kuona hali halisi ilivyo.

Naye Burhani Yakub wa Tanga anaripoti kuwa walimu wengi kwenye wilaya za mkoa huo walitumia siku ya jana kupiga soga badala ya kuingia darasani, ikiwa ni njia mojawapo ya kugoma.

Wilayani Handeni, Mwananchi imefahamishwa kuwa walimu wa baadhi ya shule zilizopo katika mji wa Chanika walitumia siku ya jana kupiga gumzo wakati wa masomo.

Wakizungumza na Mwananchi kwa sharti la kutotajwa majina yao wala shule wanazofundisha, walimu hao walisema wataendelea na mgomo baridi hadi watakapopata maelekezo mengine kwa kuwa hawana tena ari ya kufanya kazi.

Wilayani Pangani, baadhi ya walimu walisema hawako tayari kufundisha kwa sasa licha ya amri ya mahakama na kwamba wanachotaka ni serikali kuwalipa madai yao badala ya kutafuta njia za kuwatisha kwa kutumia sheria.

Kutoka Sumbawanga, Oscar Simon anaripoti kuwa walimu wilayani Mpanda waliwarejesha majumbani wanafunzi na baadaye walimu kuondoka katika vituo vyao vya kazi, wakiwaacha walimu wakuu pekee.

Mmoja wa walimu ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe, alisema kwa njia ya simu kuwa wameanza mgomo huo kama kawaida na kamwe hawataweza kutii agizo la mahakama na viongozi wao la kuacha mgomo

kwani wanaamini kuwa walimu wenyewe ndio wanapaswa kuamka na kudai haki yao.

"Tumefika shuleni kama kawaida, na baadaye tukakubaliana tunaendesha mgomo wetu kama tulivyoazimia. Hivyo tukatawanyika kwenda kuendelea na shughuli nyingine. Hii serikali si ya kucheka nayo... wao ndio vinara wa ufisadi huko juu wanataka kutukandamiza sisi kila siku kwa kutumia mgongo wa mahakama," alisema mwalimu huyo.

Mwl. Juma Kablanketi wa Shule ya Msingi Kashato mjini Mpanda alisema kuwa kimsingi wamekubaliana watakutana kesho kutathimini mgomo wao kama unaendelea au wanarejea kazini kuanzia Jumatatu ijayo.

Kutoka Kibaha, Julieth Ngarabali anaripoti kuwa vikao vya dharura vya viongozi wa CWT wa mkoa wa Pani vilipangwa kufanyika juzi maeneo ya Ruvu, Mlandizi, Kisarawe, Chalinze na Mkuranga na vilikuwa viongozwe na Mwenyekiti Kelvin Mahundi na katibu wake.

Lakini wajumbe waliojitokeza waliwaeleza viongozi hao kuwa hawaelewi kufika kwake kulikuwa na malengo gani na kushangazwa na uamuzi wa Mahakama Kuu, Kitengo cha Kazi, wa kuwataka warejee makazini.

CWT Pwani ilitoa tamko la kuridhia kutoanza mgomo kwa sharti kwamba rufaa ikatwe.

Mwenyekiti Mahumbi alisema pamoja na chama hicho kutoa tamko hilo, hana uhakika kama walimu wote watarejea kazini kwa ari ya kutekeleza majukumu yao kweli ama watakuwa wanazuga tu huko mashuleni.

Uchunguzi wa Mwananchi kwenye shule mbili za sekondari za shirika la elimu Kibaha, shule ya msingi na sekondari ya Nyumbu, Kibaha, Mwendapole, Muungano, Mkoani na Mailimoja, ulionyesha kuwa walimu wengi walikuwa wakiendelea na shughuli zao.

Jijini Dar es salaam, ambako wanachama wa CWT walizua tafrani kubwa wakati viongozi wao walipowataarifu kuwa mgomo umezuiwa, jana walionekana kama wamepungua hasira na shule nyingi zilionekana kuendelea na shughuli za elimu kama kawaida.

Ummy Muya anaripoti kuwa hali ilikuwa shwari katika shule mbalimbali za serikali, zikiwemo Forodhani na Kisutu zilizo katikati ya jiji.

"Hatuwezi kuja maeneo ya kazi na kukaa bila kufanya kazi kwa kuwa kufanya hivyo ni kuwaumiza wanafunzi na sisi mdeni wetu ni serikali kupitia wizara ya elimu," alisema mmoja kwa sharti la kutotajwa jina, lakini akageuka na kusema: "Viongozi wengi wanaisahau sekta ya elimu kwa kuwa watoto wao wanasoma nje ya nchi. Na hata kama wanasoma nchini ni katika shule za kimataifa."

Naye Furaha Kijingo anaripoti kuwa katika Shule ya Msingi Makumbusho na Victoria walimu walikuwa wakiendelea kufundisha kama kawaida.

"Hapa shuleni kwetu hali ni shwari na siwezi kuzungumza lolote kwani maelezo yote yapo kwa mkurugenzi wa manispaa," alisema mwalimu mkuu wa shule hiyo.