Wednesday, September 24, 2008

NMB Yapewa Masaa 3 Tu!!

JAJI wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Jaji Mfawidhi Ernest Mwipopo, jana alibatilisha mgomo wa wafanyakazi wa Benki ya NMB na kuwataka warejee kazini ndani ya muda wa saa tatu, uamuzi ambao umeridhiwa na wafanyakazi.

Akitoa hukumu hiyo jana, Jaji Mwipopo alizitaka pande mbili zinazopingana kutoa matangazo kwenye vyombo vyote vya habari kuwajulisha wafanyakazi hao kuwa wanatakiwa kurejea kazini kuanzia saa 11:25 jioni jana hadi leo 2:00 asubuhi.

"Aya hizo zinagongana na nafasi ya serikali kwenye madai ambayo ni msingi wa ugomvi," alisema. "Aya ya kwanza imeitaja serikali kuwa ndio iliyogoma kusaini makubaliano. Kutokana na hali hiyo kuna uwezekano kuwa mgogoro huo umeelekezwa kwa NMB kwa sababu ndio taasisi pekee mnayoweza kuigomea."

Alisema hoja ya pili inayofanya mahakama isiutambue mgomo huo na kuuita haramu na batili, ni muda wa kutolewa kwa nositi ya kuanza kwake.

Alifafanua kuwa, notisi hiyo ya saa 48 iliyotolewa Ijumaa ilimaanisha kuwa mgomo huo ulitakiwa uanze saa 10:45 Jumapili, muda ambao saa hizo 48 ulikuwa unaisha. Lakini badala yake wafanyakazi walianza mgomo huo saa 2:00 asubuhi Jumatatu.

Hali kadhalika jaji huyo alifahamisha kuwa mgomo huo ulipaswa kuanza jana na sio juzi endapo notisi yake ingetolewa kwa kutumia siku za kazi badala ya saa kwani sheria ya kazi, haitambui siku za Jumamosi na Jumapili kuwa ni siku za kazi.

"Hoja ya pili ni timing (muda), kama notisi hiyo ni ya saa 48 na ilipokewa Ijumaa saa 10:45 jioni, muda wake ungeisha saa 10:45 Jumapili. Kwa nini hamkugoma siku hiyo na mkaamua kusubiri hadi Jumatatu?" alihoji Jaji Mwipopo na kuongeza:

"Lakini ikumbukwe kwamba, sura ya kwanza ya Sheria ya Kazi... haitambui Jumamosi na Jumapili kuwa ni siku za kazi, hivyo kuhesabu siku hizo kuwa siku za kazi sio sahihi."

Kwa mujibu wa Jaji Mwipopo ni jukumu la mahakama kutafsiri notisi ya saa 48 inaisha lini, kwa kuwa sheria haikutoa tafsiri kuhusu notisi ya masaa hasa endapo notisi hiyo inatolewa mwishoni mwa juma.

"Kutokana na mambo hayo, mahakama imetengua mgomo huo na kuutangaza kuwa ni haramu na batili hivyo hautakiwi kufuatwa. Kwa mujibu wa kifungu 84 cha sheria za ajira, naamuru ndani ya masaa matatu, kuanzia sasa, wafanyakazi wote warejee kazini," alisema Jaji Mwipopo na kuongeza:

"Nimeangalia kwa makini na kugundua udhaifu wa mambo matatu ambayo yanafanya mgomo huo uonekane batili na haramu, hivyo ninatoa amri na maagizo kuhusu suala hilo.

"Naamuru mfanyakazi ambaye hakuweza kuripoti kazini leo (jana) awe ameripoti kazini kwake kesho (leo) saa 2:00 asubuhi na naagiza uongozi wa NMB uwapokee wafanyakazi hao wote bila masharti na usiwape adhabu kwa kushiriki mgomo huo."

Baada ya Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Viwandani na Taasisi za Benki (Tuico), Boniphace Nkakatisi kuwaeleza uamuzi huo, waliweka msimamo kuwa wasingerejea kazini na kumpa kiongozi huyo wakati mgumu wa kuwaelewesha.

"Nina waomba mrudi kazini kwa moyo mkunjufu tena kwa kujituma kama awali na kutii amri ya mahakama wakati sisi tunarudi mezani kwa majadiliano zaidi," alisema Nkakatisi.

Hata hivyo, hoja ya Wakili Mbwambo ilipingwa na wakili wa wafanyakazi, Khamis aliyesema: "Mheshimiwa jaji, Mbwambo hakuwa mkweli na hataki kuwa muwazi. Kutaka wafanyakazi hao warejee kazini ni kuendeleza mgogoro. Njia mwafaka ni watu kukutana na kufikia mwafaka."

Kabla ya majibizano hayo, Jaji Mwipopo alitumia muda mwingi kuwauliza maswali mawakili hao na ifuatayo ni sehemu ya mahojiano yao:

Jaji: Kwa nini, msomi Khamis, mahakama isiamini kuwa mgomvi wa Tuico ni serikali iliyokataa kusaini mabaliano yenu na sio NMB?

Wakili Khamis: Ndio maana nilisema kuna haja ya sisi kupata muda wa kuwasilisha nyaraka zetu kwa maandishi kwani makubaliano yalihusu pande tatu, wafanyakazi, NMB na serikali. Kabla ya serikali, NMB ilitakiwa iwe imesaini kwanza.

Jaji: Baada ya kutoa notisi ya saa 48 Ijumaa saa 10:45 jioni, kwa nini msingegoma Jumapili siku ambayo notisi yenu iliisha badala yake mkachagua Jumatatu?

Wakili Khamis: Sheria inataka watu wagome baada ya notisi, na kwa mujibu wa sheria hiyo hakuna ubaya watu kugoma muda wowote baada ya muda wa notisi hiyo kumalizika.

Jaji: Kwa nini masaa hayo 48 hayakuwa ya siku za kazi na hivyo kuishia Jumatatu na mgomo mkaanza leo (jana)?

Wakili Khamis: Siku za kazi sio za tarehe za mwezi, ni siku ambazo wafanyakazi wa taasisi wanatakiwa kufanya kazi na kwa NMB ni siku zote kwani ATM zinafanya kazi masaa 24, hivyo ni sahihi kuhesabu Jumamosi na Jumapili kuwa ni siku za kazi kwa NMB.

Baada ya mahojiano na wakili wa wafanyakazi, Jaji Mwipopo alimgeukia wakili wa NMB na sehemu ya mahojiano yao ni kama ifuatavyo:

Jaji: Kwa nini nyie (NMB) msionekane pia kuwa mna hila na mnashirikiana na wafanyakazi hao kuishinikiza serikali isaini makubaliano kwa kutotoa taarifa mapema kwamba Jumatatu mgomo unaanza?

Wakili Mbwambo: Tunashukuru kwamba unatukumbusha uwezekano wa kuwasiliana na ofisi yako hata siku za mwisho wa juma, lakini katika hali ya kawaida isingeweza kuwaza kwamba tungeweza kukupata siku hiyo.

Jaji: Kwa nini mnaomba viongozi hawa wakamatwe, wafilisiwe na wafungwe kama wafungwa wa madai badala ya kuomba mahakama izuie mgomo?

Wakili Mbwambo: Hili ni ombi moja tu, kumbuka pia tumeiomba mahakama ichukue hatua nyingine yoyote inayoona inafaa kunusuru hali hiyo.

Baada ya maswali na majibu hayo yaliyodumu kwa takriban saa 1:30 Jaji Mwipopo alisema: "Kuhusu maombi ya NMB kwamba viongozi wakuu wanne wasikilizwe leo na amri itolewe ya kukamatwa, kufilisiwa na kufungwa kama wafungwa wa madai, natoa amri kwamba mahakama imewapa muda ili waweze kujitetea kwa maandishi na vielelezo na kuwasilisha pingamizi la kiapo kesho, (leo) kesho kutwa wampe nakala ya hati hiyo wakili wa mwajiri na Septemba 26 tukutane hapo saa 4:00 asubuhi kuendelea na shauri hili."

Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Viwanda na Taasisi za Fedha nchini (TUICO) Boniphace Nkakatisi akiwa katika Divisheni ya Mahakama ya Kazi walipofikiswa jana kujibu mashitaka ya kuongoza mgomo wa wafanyakazi wa Benki ya NMB.

No comments: