Monday, November 3, 2008

Banda Aapishwa Kuwa Rais Zambia

Kaimu rais wa Zambia, Rupiah Banda ameapishwa kuwa rais wa nchi hiyo, masaa mawili baada ya maafisa kutangaza kuwa ameshinda kwa tofauti ya asilimia ndogo sana na mpinzani wake.

Kutokana na matokeo ya mwisho, Bw Banda amemshinda mpinzani wake mkuu Michael Sata kwa asilimia 40.1 kwa 38.1.

Hapo awali, Bw Sata alikataa matokeo hayo na kukishutumu chama tawala kwa kuiba kura.

Chama cha Bw Sata cha The Patriotic Front kimesema kitakwenda mahakamni kushinikiza kura hizo zihesabiwe upya.

Hata hivyo, waangalizi wa Jumuiya ya maendeleo na biashara ya mataifa ya kusini mwa Afrika, SADC wamesema uchaguzi huo ulikuwa wa huru na wa haki.

Chama tawala cha MMD kimesema kuwa kinatambua kuwa huu ni wakati wa wasiwasi mkubwa na hisia kali.

Lakini kimewasihi Wazambia wote kutokuwa na shaka na kufanya kazi kwa umoja na kwa amani.

Ulinzi uliongezwa mjini Lusaka kwa kuhofia kuwepo na ghasia.

Bwana Banda alichukua nafasi ya ukaimu rais mwezi Agosti kufuatia kifo cha rais Levy Mwanawasa.

No comments: