Thursday, November 6, 2008

Goma, MONUC Yajikuta Katika Mapigano

Umoja wa Mataifa umesema askari wake wamejikuta katikati ya mapigano baada ya vita kuzuka mashariki mwa DR Congo baada ya siku chache za kusitishwa mapigano.

Msemaji wa umoja wa mataifa mjini Goma amesema kumekuwepo na mapigano baina ya majeshi ya waasi na makundi mawili ya wanamgambo ambayo yanaunga mkono serikali.

Wiki iliyopita, kiongozi wa waasi Jenerali Laurent Nkunda alitangaza kusitisha mapigano wakati vikosi vyake vilipoukaribia mji wa Goma.

Mwandishi wa BBC mjini Goma, Peter Greste amesema bado kuna tishio la kuzuka upya mapigano.

Mji wa Goma umezingirwa na majeshi ya waasi ambayo yaliyafukuza majeshi ya serikali.

Watu wapatao 250,000 waliyahama makazi yao na mashirika ya misaada yanaendelea kujitahidi kuwasaidia.

Baadhi walikimbia vijiji vyao na kuelekea mjini Goma, lakini wengine wamesharudia baada ya kukosa chakula cha kutosha na mahema huko mjini.

Hapo awali, waziri wa mashauri ya kigeni wa Ufaransa alitoa wito wa kuimarisha kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa chenye askari 17,000 hivi sasa.

No comments: