Thursday, November 20, 2008

Meli ya Maharamia Yazamishwa Aden

Manuwari ya India imeangamiza meli moja ambayo inashukiwa ilikuwa na maharamia wa Kisomali, katika ghuba la Aden.

Manuwari hiyo, INS Tabar, ilibidi kuizamisha meli hiyo iliyokuwa na watu wanaoshukiwa kuwa ni maharamia, baada ya kukataa kuisimama ili meli kuchunguzwa, na badala yake walianza kufyatua risasi.

Habari hizi ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wanamaji wa India.

Kumekuwa na visa kadha vya meli kutekwa na maharamia hivi majuzi, katika pwani ya Somalia.

Kisa kilichotokea hivi karibuni kilifanyika siku chache baada ya meli ya Saudi Arabia, Sirius Star, yenye shehena ya mafuta ambayo hayajasafishwa, na wafanyakazi 25, kutekwa na maharamia na kuelekezwa kutua nanga katika pwani ya Somalia.

Sirius Star

Vela International, kampuni ambayo inasimamia safari za meli hiyo ya Sirius Star, imeielezea BBC kwamba kufikia sasa hakuna matakwa yoyote ya fidia yaliyotolewa na maharamia hao.

Kampuni hiyo pia ilielezea kwamba wafanyakazi wa meli hiyo wote wako salama.

Meli hiyo imebeba mapipa milioni mbili ya mafuta ambayo hayajasafishwa, na yenye thamani ya dola milioni 100 za Kimarekani.

No comments: