Thursday, November 20, 2008

Wafungwa wapigwa vibaya mno Kenya


Msemaji wa idara ya magereza nchini Kenya, amesema ameshangazwa na video ambayo inaonyesha maafisa wa magereza wakiwapiga kikatili wafungwa gerezani, na uchunguzi umeanzishwa mara moja kuhusiana na tukio hilo.

Mfungwa mmoja alifariki kutokana na ukatili huo, na wafungwa wenzake wanasema kifo hicho kilitokana na kipigo alichofanyiwa na maafisa wa magereza.

 Yeyote anayezingatia haki za kibinadamu atashtushwa na yaliyotokea
 
Dickson Mwakazi msemaji wa Idara ya Magereza nchini Kenya

Picha hiyo ya video iliyonaswa kwa kutumia simu ya mkononi, inaonyesha wafungwa walio uchi katika jela yenye ulinzi mkali ya Kamiti, wakitandikwa kwa rungu na mijeledi.

Haijafahamika kama picha hizo zilipigwa na mfungwa au afisa wa magereza aliyekuwa na huruma.

Wafungwa hao walipigwa wakati maafisa wa magereza walikuwa wakiendesha oparesheni ya kuwapokonya simu wafungwa.

Wafungwa nchini Kenya hawaruhusiwi kumiliki au kutumia simu.

No comments: